RAIS UFARANSA AHIMIZA CHANJO AFRIKA

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa(kulia) akimpongeza mwenzake Rais Emmanuel Macron baada ya mkutano wa pamoja na waandishi wa habari Pretoria.

***********

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron anasema angependelea kuona asilimia 60 ya Waafrika wamepewa chanjo ya kupambana na ugonjwa wa COVID-19 ifikapo katikati ya mwaka 2022.

 Akizungumza na Wafaransa wanaoishi huko Afrika Kusini kiongozi huyo wa Ufaransa alisisitiza juu ya umuhimu wa ushirikiano wa karibu kati ya Afrika na Ulaya kufikia malengo ya maendeleo.


Kabla ya Hapo Macron alitoa heshima zake kwa rais wa kwanza muafrika wa nchi hiyo Nelson Mandela kwa kutembelea ofisi za wakfu yake mjini Johanesburg.

Macron alimsifu kiongozi huyo shujaa mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel kwa kujitolea muhanga kutetea usawa na haki na kusema kazi zake hazikuwanufaisha Wafrika Kusini pekee bali dunia nzima.

Siku ya Ijumaa katika Chuo Kikuu cha Pretoria pamoja na Waziri wa Afya wa Ujerumani Jens Spahn na Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini, walizindua mpango mpya wa uwekezaji wa kutengeneza chanjo barani Afrika.

Macron amesema mradi huo utafadhiliwa na nchi za Umoja wa Ulaya, Marekani na Benki kuu ya Dunia, na kwamba wanataka kubadilishana teknolojia na kufunguliwa kwa viwanda vya kuzalisha chanjo katika sehemu mbali mbali za Afrika.

Rais Ramaphosa amesema changamoto kubwa na ya hatari kwa nchi za Afrika ni kuweza kupata hizo chanjo ambazo anasema zimejaa katika nchi zilizoendelea wakati nchi maskini zinapata sehemu ndogo sana ya chanjo hizo.

Post a Comment

0 Comments