Mahakama nchini Kenya imeshtaki wanaume wawili akiwemo raia wa China kwa tuhuma za kusafirisha siafu kinyume cha sheria, tukio linaloibua mjadala kuhusu biashara hii isiyozoeleka lakini yenye thamani kubwa kimataifa.
Tukio hilo lilitokea Machi 17, 2026 baada ya Zhang Kequn (27) kukamatwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta jijini Nairobi akiwa na zaidi ya siafu 2,000, akijaribu kuondoka nchini humo.
Kwa mujibu wa nyaraka za mahakama, Zhang alikuwa tayari amewekewa alama maalum kwenye hati yake ya kusafiria kufuatia tuhuma za kukwepa kukamatwa mwaka 2025.
Mamlaka ya Wanyamapori Kenya imesema ukusanyaji na usafirishaji wa siafu bila kibali ni kosa la kisheria, kwani ni ukiukwaji wa sheria za bayoanuwai pamoja na kanuni za kimataifa za uhifadhi wa viumbe hai.
Katika kesi hiyo, mtu wa pili, Charles Mwangi, naye ameshtakiwa kwa tuhuma za kukusanya na kusambaza siafu kwa wafanyabiashara wa kigeni.
Akijitetea mahakamani, wakili wa Zhang, David Lusweti, amesema mteja wake alikuwa akisafirisha siafu hao bila kuwa mmiliki wake, akidai kuwa Mwangi ndiye aliyekuwa akikusanya na kuuza wadudu hao.
Uchunguzi wa maafisa wa usalama umebaini kuwa Mwangi anahusishwa pia na mzigo mwingine wa siafu uliokamatwa Bangkok Machi 10, uliokuwa umetokea Mombasa nchini Kenya.
Kwa nini siafu wanakuwa bidhaa?
Licha ya kuonekana wadudu wa kawaida, siafu wamegeuka kuwa bidhaa inayotafutwa sana katika masoko ya kimataifa, hasa Asia na Ulaya.
Wafugaji wa siafu hutumia wadudu hao kwa ajili ya maonesho, tafiti za kisayansi, pamoja na burudani ambapo watu hujenga makazi maalum ya siafu (ant farms) na kuzifuga kama wanyama wa kufurahisha.
Aidha, baadhi ya watu huamini kuwa kuangalia siafu wakifanya kazi katika makoloni yao husaidia kupunguza msongo wa mawazo.
Hata hivyo, wataalamu wanaonya kuwa biashara hii inapofanywa kiholela inaweza kuhatarisha mifumo ya ikolojia, kusababisha upotevu wa spishi na kueneza siafu vamizi katika maeneo mapya.
Kesi hii inaonyesha kuongezeka kwa mtandao wa biashara haramu ya viumbe hai, huku mamlaka zikisisitiza udhibiti mkali ili kulinda rasilimali za asili.

0 Comments