WORLDVISION MKINGA YAPONGEZWA KWA MIRADI YA AFYA|ELIMU NA CHAKULA

 

Moja ya Darasa lililokabidhiwa kwa Mkuu wa wilaya ya Mkinga Kanali Maulidi Surumbu,hafla iliyofanyika katika kijiji cha Mazola.

Mratibu wa Worldvision Tanzania katika wilaya ya Mkinga Evodia Shija akiwa na Mkuu wa wilaya ya Mkinga Kanali Maulidi Surumbu kwenye uzinduzi wa choo cha Wanafunzi.
MKUU wa Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga Kanal Maulid Sulumbu
Mratibu wa Worldvision Mkinga Evodia Shija
Wanachi waliojitokeza wakifuatilia kwa ukaribu shughuli zinavyoendelea Mazola.

*******************

MKUU wa Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga Kanal Maulid Sulumbu amepokea miradi ya zaidi ya Millioni 800 kutoka shirika la Worldvision Tanzania.

Kanali Maulid Sulumbu amesema kukabidhiwa kwa miradi 18 ya madarasa,afya, maji,lishe na usafi wa mazingira miradi ambayo imegarimu zaidi ya shilingi milioni 800.

Kanali Sulumbu amelishukuru shirika la World vision kwa kutoa kiasi hicho cha fedha kwa ajili ya kutatua changamoto zinazoikabili jamii  kwenye wilaya hiyo jambo ambalo wadau wengine wa maendeleo wanapaswa kuliiga. 

"Mchango wao ni mkubwa kwa kuwa umeweza kuchangia upungufu wa madarasa tulio nao katika shule za msingi wameweza kutupunguzia adha ile ya kuwa na upungufu wa madarasa zaidi ya 2000 na sasa ivi tunazungumzia upungufu wa madarasa 1500 na wako tayari kuendelea kutusaidia kwenye sekta hii pale ambapo watapata uwezo"alisisitiza Kanal Sulumbu.

Aidha Kanali Sulumbu amesema Wilaya ya Mkinga ni miongoni mwa Wilaya za Mkoa Tanga ambazo zilipata upungufu wa chakula ikiwemo Wilaya ya Handeni na Mkinga ambapo mwaka jana shirika hilo liliweza kupeleka chakula mashuleni jambo ambalo limekwenda kuongeza ufaulu. 

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo,Elizabeth Dickson amesema miradi inakwenda kuwanufaisha wana Mkinga hivyo wao kama Halmashauri wapo tayari kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kuhakikisha adhma ya serikali ya kuwahudumia wananchi kwa kutoa huduma bora na zenye hadhi inayotakiwa kulingana na kauli mbiu ya mheshimiwa Rais wao kama Halmashauri wanaitimiza na kuitekeleza ipasavyo. 

"Kwetu sisi ni faraja kuwepo kwa miradi hii kwanza inakwenda kuongeza ufaulu kwa watoto lakini pia inakwenda kuimarusha afya za watoto kupitia vyakula wanavyovipata mashuleni pia uhakika wa usalama wa maji vile vile miradi hii inakwenda kuongeza tija kwa wananchi na kupunguza kiwango cha utoro kwa wanafunzi hivyo kwetu kama Halmashauri ni faida kubwa sana, "alisema Kaimu Mkurugenzi. 

Mratibu wa Worldvision Mkinga Evodia Shija amesema miradi hiyo inalenga kuweka mazingira rafiki kwenye sekta ya elimu, maji na afya.

Evodia amesema kuwa shirika hilo la Worldvision linafanya kazi katika maeneo yote bila kujali dini,  kabila wala ubaguzi wa aina yeyote ile hivyo wanashirikiana na serikali kuboresha miundombinu ambayo inamfanya mtoto aweze kuishi kwa furaha. 

"Miradi ya leo tuliyokabidhi ni 18 ikiwemo vyoo,  madarasa,  zahanati,  mradi wa umwagiliaji lengo tunataka kuboresha mazingira ya jamii zetu kwa kuwasaidia kuondokana na adha mbalimbali zinazowakabili katika maeneo yao, "alisema Evodia. 

Wanafunzi wa shule ya msingi Mazola akiwemo Asha Hassan na Mohamed Omari wameonesha furaha yao kupata madarasa matano yanayokwenda kuwaondolea adha ya kukaa chini pamoja na kuondoa utoro kwa wanafunzi  shuleni hapo.

Miradi hiyo 18 yenye zaidi ya shilingi milioni 800 imetekelezwa na shirika hilo kwenye Wilaya hiyo ya Mkinga  na kwamba uhitaji huo  pia unaonekana kwenye tarafa nyingine zilizopo kwenye wilaya hiyo jambo ambalo wadau wa maendeleo wanapaswa kuliunga mkono.

Post a Comment

0 Comments