MWALIMU SHULE YA TLAWI MATATANI

Naibu waziri wa ofisi ya Rais TAMISEMI David Silinde amemsimamisha kazi mkuu wa shule ya sekondari ya Tlawi iliyopo wilaya ya Mbulu mkoa wa Manyara na kuagiza uchunguzi ufanyike juu yake baada ya kumdanganya gharama za ununuzi wa saruji na ujenzi wa bweni.

Hatua hiyo imekuja baada naibu waziri huyo kufika katika shule hiyo kufanya ukaguzi wa thamani ya fedha katika miradi ya lipa kwa matokeo ambapo kwa shule ya Tlawi wao walipewa ujenzi wa madarasa matatu,bweni na choo kwa gharama ya milioni 148.8 na kugundua kuwa fedha iliyotumika katika ununuaji wa vifaa ni nyingi tofauti na bei halisi huku akitolea mfano wa bei aliyoambiwa na mkuu wa shule hiyo kuwa saruji walinunua kwa bei ya jumla ya shilingi 18000 kwa mfuko ambayo si kweli na kwani bei ya jumla ya kiwandani ambayo haizidi shilingi 13000-14000 pamoja na usafirishaji.

Katika hatua nyingine Naibu waziri Silinde ameagiza kuvunjwa kwa kamati ya ujenzi wa shule hiyo kwa kushindwa kusimamia ujenzi na kuagiza iundwe mpya kamati nyingine haraka,huku afisa elimu sekondari akitakiwa kuandika barua ya kwanini ameshindwa kusimamia mradi huo na kwanini asichukuliwe hatua za kinidhamu.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mbulu Chelestino Mofuga amesema amepokea maelekezo ya Naibu waziri silinde na kuagizia kwa kamanda wa TAKUKURU wilaya hiyo kuanza uchunguzi mara moja wa matumizi ya fedha za ujenzi huo na kupelekewa ripoti ambayo ataifikisha katika ofisi ya TAMISEMI.

Mbunge wa Jimbo la Mbulu mji Zacharia Paul Isaay amesema gharama iliyotumia katika ujenzi wa bweni si ya kweli na haiendani na thamani halisi ya bei na kuomba uchunguzi maalum katika miradi wilayani mbulu huku akiiomba serikali itazame upya kuwasaidia wananchi kumalizia majengo hayo.

Post a Comment

0 Comments