WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene amesema Rais Samia Suluhu,ametoa ajira mpya za askari 2,300 kwa vyombo vyote vya usalama vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.
“Napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya Wizara na Vyombo hivi ambavyo Wizara yetu inavisimamia kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupatia nafasi hizi, pamoja na changamoto tulizokuwa navyo, suala la upungufu wa askari lilikua jambo ambalo linatupa changamoto, na uzuri ni kwamba kibali kilichokuja kutoka Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma kimeelekeza kabisa tuajiri askari wa ngazi ya chini,” alisema Simbachawene.
Aliongeza kuwa, askari hao ndio watakuwa wapiganaji, wapambanaji, na anatarajia kuwa vyombo hivyo katika mchakato wake vitazingatia maelekezo ya Serikali ya kuhakikisha kwamba watakaopata nafasi hizo ni wale waliopitia Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kupata malezi na kuhitimu lakini pia walishiriki katika kujenga nchi kupitia JKT.

0 Comments