MGOMBEA UBUNGE WA CCM TANGA MJINI AAHIDI KUKAMILISHA UJENZI WA SOKO LA MAKOKORORA

Mgombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM),Kassim Amari akiwasili kwenye mkutano wake wa kampeni Kata ya Makorora


Mgombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM),Kassim Amari akizungumza kwenye mkutano wake wa kampeni Kata ya Makorora

*************

TANGA MJINI

Mgombea ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kassim Amari, amewaahidi wananchi wa Tanga Mjini kuwa atahakikisha Soko la Makorora linakamilika kwa wakati, jambo ambalo litaleta tija kwa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika Kata ya Makorora, Amari alisema soko hilo litawawezesha wafanyabiashara kufanya biashara katika mazingira salama na yenye mpangilio wa kisasa.

 “Soko la Makorora ni miongoni mwa miradi iliyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025–2030, hivyo ni lazima likamilike kwa wakati,” alisema Amari.

Aliongeza kuwa Soko la Mlango wa Chuma pia litajengwa kuwa soko la kisasa, huku Soko la Mgandini likibadilishwa kabisa na kuwa na sura mpya itakayovutia wananchi na wafanyabiashara.

Mgombea huyo pia alisema kuwa ili kupunguza kero zinazotokana na bili kubwa za maji, wakazi wote watabadilishiwa mita za maji na kufungiwa mita za luku za maji, zitakazowawezesha kulipia matumizi kulingana na kiasi wanachotumia.

Amari alisisitiza kuwa CCM chini ya uongozi wa Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan inajipanga kutekeleza Ilani ya Uchaguzi kupitia miradi inayoleta manufaa kwa wananchi moja kwa moja.

Aliwaomba wananchi wa Tanga Mjini kuichagua CCM kuanzia ngazi ya udiwani, ubunge hadi urais ifikapo Oktoba 29,akisisitiza kuwa ahadi zote zilizopo katika kampeni zinaungwa mkono na ilani ya chama hicho.

Post a Comment

0 Comments