Rais wa Kenya William Ruto amesema nchi za Afrika Mashariki zinaendelea kujadili mpango wa kuanzisha kiwanda cha pamoja cha kusafisha mafuta katika bandari ya Tanga, Tanga, ili kupunguza utegemezi wa bidhaa za petroli kutoka nje ya ukanda huo.
Akizungumza Alhamisi jijini Nairobi katika mkutano wa ufadhili wa miundombinu, Ruto amesema kwa sasa nchi za Afrika Mashariki zinaagiza bidhaa zote za mafuta yaliyosafishwa kutoka nje, hususan Mashariki ya Kati, hali inayozifanya kuwa katika hatari ya kukumbwa na changamoto za upatikanaji na kupanda kwa bei, hasa wakati wa migogoro ya kimataifa.
Ameeleza kuwa kiwanda hicho kinatarajiwa kuhudumia nchi kadhaa za ukanda huo kwa kusafisha mafuta yatakayotoka katika mataifa mbalimbali ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Kenya, Sudan Kusini na Uganda.
Kwa upande wake, tajiri mkubwa barani Afrika, Aliko Dangote, amesema yuko tayari kuwekeza katika mradi huo kwa kuiga mfano wa kiwanda chake cha kisasa cha kusafisha mafuta nchini Nigeria, iwapo serikali za ukanda huo zitatoa ushirikiano unaohitajika.
Dangote amesema kuwa endapo makubaliano yatafikiwa na nchi tatu au nne za Afrika Mashariki, kampuni yake iko tayari kuongoza utekelezaji wa mradi huo na kuhakikisha kiwanda hicho kinajengwa ndani ya kipindi cha miaka minne hadi mitano.
Wakati huo huo, Uganda nayo imeendelea na mipango ya kujenga kiwanda chake cha kusafisha mafuta, huku ikitarajia kuanza uzalishaji wa mafuta ghafi kwa biashara. Tayari mwaka 2024, nchi hiyo ilisaini makubaliano na kampuni ya Alpha MBM Investments yenye makao yake Umoja wa Falme za Kiarabu kwa ajili ya kuendeleza kiwanda chenye uwezo wa kuchakata mapipa 60,000 kwa siku.
Mbali na sekta ya mafuta, Dangote pia ametangaza mpango wa kuanzisha takriban vituo 20 vya kuchanganya mbolea barani Afrika ifikapo mwaka 2028 ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya pembejeo za kilimo.
Aidha, akizungumzia mpango wa kuorodhesha kiwanda chake cha kusafisha mafuta nchini Nigeria, Dangote amesisitiza umuhimu wa wawekezaji wa Kiafrika kushiriki, akieleza kuwa bara hilo linapaswa kunufaika moja kwa moja na miradi mikubwa ya kimkakati, huku akiahidi kulipa gawio kwa dola za Marekani.

0 Comments