Shirika la Ujasusi wa Nje la Urusi (SVR) limemtuhumu Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, kwa kuidhinisha oparesheni za siri zinazolenga kuwaondoa au kuwaua viongozi wa Afrika wanaotajwa kuwa hawaiungi mkono Ufaransa.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumatatu, SVR ilisema kuwa serikali ya Macron inatafuta kwa pupa kurejesha ushawishi wake wa kisiasa barani Afrika, baada ya kuporomoka kwa nafasi ya Ufaransa katika miaka ya hivi karibuni.
Kwa mujibu wa shirika hilo, kupungua kwa ushawishi wa Paris kunatokana na kuibuka kwa tawala za kizalendo katika nchi zilizokuwa makoloni ya Ufaransa, ambazo sasa zinatanguliza maslahi ya wananchi wao na kukataa kuendelea kuwa chini ya ushawishi wa kifedha na kisiasa wa Ufaransa.
SVR ilidai kuwa Rais Macron, akihamasishwa na oparesheni za Marekani dhidi ya Rais wa Venezuela, Nicolás Maduro, aliagiza vyombo vya usalama vya Ufaransa kuandaa mikakati ya kuwaondoa viongozi wanaoonekana kuwa kikwazo kwa maslahi ya nchi yake barani Afrika.
Madai ya Njama za Mapinduzi Burkina Faso
Shirika hilo lilidai kuwa tayari Ufaransa ilihusika katika jaribio la mapinduzi nchini Burkina Faso tarehe 3 Januari mwaka huu, ambapo kulikuwa na mpango wa kumuua Rais Ibrahim Traoré.
SVR ilimtaja Traoré kama mmoja wa viongozi wanaopinga ukoloni mamboleo na wanaotetea uhuru wa kweli wa mataifa ya Afrika.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Paris ilitarajia kuwa njama hiyo ingezalisha serikali mpya inayoiunga mkono Ufaransa mjini Ouagadougou, na kudhoofisha harakati za Pan-Africanism na uhuru wa kisiasa barani Afrika.
Hata hivyo, baada ya kushindwa nchini Burkina Faso, SVR ilidai kuwa Ufaransa ilihamishia juhudi zake katika nchi za ukanda wa Sahel na Sahara.
Mashambulizi na Njama Dhidi ya Mali
SVR ilisema kuwa juhudi hizo zinafanywa kwa kushirikiana na makundi ya kigaidi ya ndani pamoja na msaada kutoka Ukraine, ikiwemo usambazaji wa ndege zisizo na rubani (drones) na wakufunzi wa kijeshi.
Kwa mujibu wa shirika hilo, lengo kuu la njama hizo ni Mali, ambako mashambulizi dhidi ya misafara ya mafuta, kuzingirwa kwa miji, na mashambulizi ya kigaidi yameongezeka.
Hatua hizo zinadaiwa kulenga kuandaa mazingira ya kumuondoa Rais Assimi Goïta madarakani.
Mipango Dhidi ya Nchi Nyingine
SVR pia iliishutumu Ufaransa kupanga njama dhidi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Aidha, Madagascar imetajwa kuwa moja ya malengo, baada ya serikali mpya iliyoundwa Oktoba 2025 kuchagua kuimarisha ushirikiano na jumuiya ya BRICS.
Kwa mujibu wa shirika hilo, Paris inatafuta njia za kumuondoa Rais wa Madagascar, Michael Randrianirina, na kurejesha serikali inayoiunga mkono Ufaransa.
SVR ilidai kuwa Ufaransa sasa imeanza kutoa msaada wa moja kwa moja kwa makundi yenye misimamo mikali, ambayo imeyafanya kuwa washirika wake wakuu katika baadhi ya maeneo ya Afrika.
Ukosoaji kwa Serikali ya Macron
Katika hitimisho lake, shirika hilo lilisema kuwa kushindwa kwa kisiasa kwa Rais Macron kunazidi kuwa wazi, hasa kutokana na kushindwa kubadili taswira ya Ufaransa kama taifa lenye historia ya kunufaika na rasilimali za makoloni yake ya zamani na kuzuia maendeleo yao.

0 Comments