Mwakilishi wa Kudumu wa Urusi katika Umoja wa Mataifa, Vassily Nebenzya, amesema kuwa Moscow inatarajia Marekani itatumia busara na hekima katika kushughulikia suala la Iran, akionya dhidi ya matumizi ya nguvu za kijeshi ambayo yanaweza kuhatarisha usalama wa kimataifa.
Akizungumza kuhusu mvutano unaoendelea kati ya Marekani na Iran, Nebenzya amesema kuwa hatua zozote za kijeshi dhidi ya Tehran hazikubaliki na zinaweza kusababisha madhara makubwa kwa ukanda wa Mashariki ya Kati na dunia kwa ujumla.
Amesisitiza kuwa Urusi inaamini katika suluhu za kidiplomasia na mazungumzo ya amani, na inatarajia viongozi wa Marekani kuachana na mpango wa kutumia nguvu za kijeshi kama njia ya kutatua mgogoro huo.
Kauli ya Urusi imekuja kufuatia matamshi ya Rais wa Marekani, Donald Trump, aliyoyatoa Januari 28, ambapo alirejesha vitisho dhidi ya Iran na kutangaza uwepo wa meli ya kubeba ndege ya Abraham Lincoln katika maji ya eneo hilo.
Katika kauli yake, Trump alisema kuwa “meli kubwa inaelekea Iran,” kauli iliyotafsiriwa kama onyo la kijeshi kwa Tehran.
Kwa upande wake, Balozi wa Iran katika Umoja wa Mataifa, Amir Saeed Iravani, ameandika barua kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Rais wa Baraza la Usalama, akilaani vikali matamshi ya Trump na kuyataja kuwa ya kuchochea vita na kinyume na sheria za kimataifa.
Iravani amesema kauli hizo zinakiuka misingi ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa na hazioneshi uwajibikaji wa kidiplomasia unaotarajiwa kwa viongozi wa mataifa makubwa.
Wachambuzi wa masuala ya kimataifa wanasema kuwa katika muhula wa pili wa urais wa Donald Trump, sera ya Marekani kuelekea Iran imeendelea kuwa ya misimamo miwili, ikijumuisha vitisho vya kijeshi na shinikizo la kiuchumi, huku wakati huo huo ikionesha nia ya kufanya mazungumzo.
Kwa mujibu wa wachambuzi hao, mkakati huo unalenga kuilazimisha Iran kukubali masharti ya Washington, jambo ambalo linaongeza mvutano na kutishia amani ya kikanda na kimataifa.
Urusi imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuheshimu diplomasia, sheria za kimataifa na kuhifadhi amani, ikionya kuwa mzozo wowote wa kijeshi dhidi ya Iran unaweza kuwa na athari zisizotabirika.

0 Comments